Jumatatu, 8 Februari 2016

Uhusiano wa Sintaksia na Matawi mengine ya Isimu



Dhana ya sintaksia imejadiliwa na wanazuoni mbalimbali ;
            Massamba na wenzake (1999:34) anasema “sintaksia ni utanzu wa sarufi unaojihusisha na uchunguzi wa mpangilio wa maneno katika sentensi na uhusiano wa vipasho vyake”. Wanaendelea kusema, utanzu huu huchunguza sheria  au kanuni zinazofuatwa katika kuyapanga maneno ili yalete maana inayokubalika na kueleweka katika lugha husika.
           Habwe na Karanja (2004) wanasema “sintaksia ni utanzu wa isimu unaoshughulikia muundo wa sentensi na elementi nyingine zinazounda sentensi kama vile kategoria za maneno, vikundi na vishazi”
        TUKI (2004)anasema “sintaksia ni tawi la isimu linaloshughulikia uchanganuzi wa taratibu na kanuni za mahusiano baina ya maneno katika tungo” kwa ufupi sintaksia ni tawi la isimu ambalo linachunguza muundo wa tungo pamoja na uhusiano wa vipashio hivyo vinavyounda tungo ambayo ni nukta pacha, neno, kirai na kishazi.
           Kwa ujumla sintaksia ni tawi la isimu ambalo linahusu namna maneno yanavyoungana na kuhusiana kirai, kishazi na sentensi. Sintaksia inachunguza namna maneno yanavyojipanga katika sentensi kwa kuzingatia kanuni za sarufi ya lugha husika.
         Kwa hiyo kutokana na kwamba sintaksia pia ni kitengo mojawapo kinachounda maarifa ya lugha, kwamba, sintaksia haiwezi kutenganishwa na vitengo vingine vya lugha kutokana na uhusiano mkubwa uliopo baina ya vitengo hivi. Vitengo hivi hutegemena na kuathiriana. Hivyo basi tunaweza kuonesha jinsi sintaksia isivyoweza kutenganishwa na vitengo vingine vya lugha yaani fonolojia, mofolojia na semantiki kama ifuatavyo:
Uhusisno uliopo kati ya sintaksia na fonolojia.
          Massamba na wenzake (1999:34) wanasema “fonolojia ni uchambuzi wa mfumo wa sauti katika lugha mahususi” Ni jinsi ambavyo vitamkwa au sauti za lugha zinavyoungana ili kujenga maneno yanayokubalika katika lugha. Ni dhahiri kwamba kuna uhusiano usio na mashaka kati ya sintaksia na fonolojia kwa sababu hatuwezi kuwa na miuundo mikubwa bila kuwa na mpangilio sahihi wa sauti katika lugha.
Mfano 1. ‘anacheza’ hili ni neno lakini pia ni sentensi, hivyo linaweza kuchanganuliwa            kifonolojia kama, /a/n/a/ch/e/z/a/. kwa hiyo mpangilio sahihi wa sauti hizo ndizo zinazounda neno ‘anacheza’.
Mfano 2 (a). neno “debe” neno hili limeundwa na konsonanti irabu konsonanti irabu (KIKI).
           2. (b). “edbe” hili limeundwa na irabu konsonanti konsonanti irabu (IKKI).
Katika mfano 2a, neno “debe” lina maana na limefuata kanuni na mpangilio unaokubalika katika lugha ya Kiswahili, lakini katika mfano 2b neno “edbe” halina maana katika lugha ya Kiswahili kwa sababu halina mpangilio sahihi wa vitamkwa au fonimu.
Kwa hiyo mpangilio sahihi wa sauti katika maneno ndio husaidia kupata vipashio vikubwa zaidi katika lugha kama vile kirai, kishazi na sentnsi. Kwa hiyo sintaksia na fonolojia haviwezi kuenganishwa.
Uhusiano uliopo kati ya sintaksia na semantiki.
        Habwe na Karanja wakimnukuu Richard na Wenzake (1985) wanasema “Semantiki ni stadi ya maana. Semantiki ni utanzu unaochunguza maana katika lugha ya mwandamu”. Wanaendelea kusema semantiki hutafiti maana za fonimu, mofimu, maneno na tungo. Hivyo kutokana na fasili hii maana hushughulikiwa katika vitengo au viwango vyote vya lugha ambavyo ni fonolojia, mofolojia na sintaksia. Kwa mfano,
1               Mtoto mtiifu amefaulu mtihani.
2                Mtihani mtoto amefaulu mtiifu.
3              Mtiifu mtoto mtihani amefaulu.
Katika mifano hii sentensi (1) ina maana kutokana na kwamba imefuata mpangilio sahihi wa maneno katika tungo na sentesi zilizobaki hazina maana kutokana na sababu kwamba hazijafuata mpangilio ulio sahihi wa kimuundo katika lugha ya Kiswahili. Kwa mantiki hii, kwa kuwa semantiki hushughulikia viwango vyote vya lugha, basi hushughulikia pia kiwango cha sintaksia ambapo huangalia maana za tungo, kwani tungo lazima ikubalike kwa wazungumzaji wa lugha husika, pia tungo lazima ilete maana. Kwa mantiki hiyo kuna uhusiano usio na mashaka kati ya sintaksia na semantiki kwa sababu mpangilio sahihi wa maneno katika sentensi ndiyo huleta maana na bila mpangilio sahihi wa maneno maana hupotea.
Uhusiano uliopo kati sintaksia na mofolojia.
        Besha (2007:49) anasema “mofolojia ni taaluma inayojishughulisha na kuchambua muundo wa maneno katika lugha’.Pia Rubanza (1996:1) anasema “mofolojia ni taaluma inayoshughulikia vipashio vya lugha katika kuunda maneno”. Maumbo ya kimofolojia huathiri vipengele vingine vya kisintaksia kama vile kipengele cha umoja na wingi, katika maumbo ya kimofolojia ndicho kinachoathiri umbo linalofuata jina na kuathiri muundo wa sentensi nzima. Kwa mfano,
1                        Mtoto alikuwa anajifunza kusoma.
2                        Watoto walikuwa wanajifunza kusoma.
Katika mifano hii kiambishi m- na wa- katika upande wa kiima vimeathiri utokeaji wa viambishi a- na wa- katika upande wa kiarifu. Hivyo taaluma ya sintaksia na mofolojia haziwezi kutenganishwa.
            Kwa ujumla sintaksia kama tawi mojawapo la isimu linauhusiano wa moja kwa moja na matawi mengine kwani haiwezi kutenganishwa na vitengo vingine vya lugha kutokana na uhusiano mkubwa uliopo baina ya vitengo hivi. Hutegemeana na kuathiriana kwa kiasi kikubwa, mfano huwezi kupata mofolojia bila kupitia ngazi ya fonolojia na pai huwezi kuwa na ngazi ya sintaksia bila kupitia ngazi ya fonolojia na mofolojia lakini vitengo vyote hivi hutawaliwa na kitengo cha semantiki ili kuleta mawasiliano miongoni mwa wazungumzaji.






                                          MAREJEO
Besha, R.M. (2007). Utangulizi wa Lugha na Isimu. Dar es Salaam: Mackmillan Aidan
Habwe, J na P. Karanja (2004). Misingi ya Sarufi ya Kiswahili. Nairobi: Phoenix Publishers Ltd.
Massamba, D.P.B na wenzake (1999). Sarufi Miundo ya Kiswahili Sanifu: Sekondari na Vyuo.          Dar essalaam: TUKI.
Rubanza, Y.I (1996). Mofolojia ya Kiswahili. Dar es salaam: Chuo Kikuu Huria cha Tanzania.
TUKI (2004). Kamusi ya Kiswahili Sanifu. Dar es salaam: TUKI.

Dhana ya Nadharia



Dhana ya nadharia imejadiliwa na wanazuoni mbalimbali ambao wamekuja na mitazomo tofauti tofauti kama ifuatavyo;
           Kwa mujibu wa Wamitila, (2003:22) “nadharia ni mawazo, dhana au maelezo yanayotolewa kuelezea hali fulani : chanzo chake, muundo wake, utenda kazi wake na mwingiliano wake wa ndani na nje”
          TUKI (2004:300) wanasema “nadharia ni mawazo, maelezo au mwongozo uliopangwa ili kusaidia kueleza, kutatua au kutekeleza jambo fulani”
Fasili hii ya TUKI inafanana kwa kiasi fulani na fasili ya Mdee (2011) anayefasili nadharia kuwa ni mpango wa maneno uliotungwa ili kuelekeza jinsi ya kufanya au kutekeleza  jambo fulani. http://kapeleh.blogspot.com/2014/05/nadharia-za-maana.html
Kwa msingi huo nadharia hubeba mawazo ,dhana au maelezo yatolewayo kwa nia au lengo la kueleza hali fulani, chanzo,muundo, utendaji na mwingiliano wa ndani na nje.
Kuna nadharia mbalimbali ambazo zimejadiliwa na wanazuoni mbalimbali, baadhi ya nadharia hizo ni pamoja na nadharia ya maana, nadharia za kifalsafa, kihistoria, nadharia ya fasihi, nadharia za chimbuko la lugha ya Kiswahili, nadharia ya chimbuko na chanzo cha lugha.
             Naye Wafula  na Njogu (2007:7) wamefasili dhana ya nadharia kama ni jumla ya maelekezo yanayomsaidia msomaji au mhakiki kuifahamu kazi ya fasihi kwa kufuata utaratibu maalumu. Fasili hii imeegemea hasa katika nadharia ya uhakiki wa fasihi. Pia imetaja vitu muhimu kama vile, maelekezo ambayo ndiyo yanamuongoza msomaji au mhakiki ili asivuke mipaka ya mawazo ya hiyo nadharia aitumiayo ili kufanikisha kazi kwa ufasaha.
               Pia Sengo (2009:1) anafasili nadharia kuwa ni wazo kuu fikra kuu, mwongozo mkuu wa mtu, watu au jamii ya pahala fulani, wakati fulani na kwa sababu fulani. Kwa mantiki hiyo nadharia ni dira au mwongozo wa kulikabili jambo kifalsafa, kidini, kimantiki, kijamii na kiutamaduni.
             Ili kuweza kudhibitisha maelezo yaliyotolewa na wataalamu mbalimbali kuhusu dhana ya nadharia ni vyema kuangalia mfano mmojawapo wa nadharia, ambayo ni nadharia ya sarufi. Katika nadharia hii kuna wanaisimu mbalimbali wamejitokeza kuelezea nadharia ya sarufi kwa mitazamo tofauti tofauti ambayo imeweza kuibua nadharia mbalimbali za sarufi kama vile nadharia ya sarufi mapokeo, nadharia ya sarufi msonge na nadharia ya miundo virai.
                Katika nadharia ya sarufi mapokeo Mgullu (1999:68) anasema ni sarufi ya kale iliyochambuliwa kwa kutumia vigezo vya lugha za Kilatini na Kigiriki zilizokuwa na mnasaba mmoja, yaani zilikuwa na asili moja. Kwa mantiki hiyo lugha za Kilatini na Kigiriki zilikuwa kama kiolezi cha kuchanganulia lugha nyingine ikiwemo lugha ya Kiswahili. Kwa mfano wanaisimu wa Kilatini waliposema kuna aina nane za maneno na baadhi yao katika lugha ya Kiswahili wakasema kuna aina nane za maneno bila kuzingatia kwamba lugha hutofautiana. Pia nadharia hii ilijikita na sentensi sahili, haikujishughulisha na miundo  kwa marefu na mapana.
              Baada ya kuonekana sarufi mapokeo ina udhaifu mkubwa iliibuka nadharia ya sarufi msonge. Mgullu (1999:70) anaiona sarufi hii ni sehemu ya mkabala wa kimapokeo isipokuwa mkabala huu unaiona lugha kuwa ni mfumo mkuu yenye mifumo mingi ndani yake kama vile mifumo midogo ya fonolojia, mofolojia, sintaksia na semantiki.
             Katika karne ya kumi na nane na kumi na tisa sarufi mapokeo ikafikia kilele ndipo ikaibuka nadharia ya sarufi miundo virai. Nadharia hii inadokeza kuwa tungo imeundwa na viambajengo ambavyo vina uhusiano na vipo kidarajia. Kwa mujibu wa Mgullu (1999:70) isimu muundo imejitokeza sana katika maandishi ya akina Harris, Ferdinand De Saussure, Trubetzkoy na Bloomfield.
Katika mkabala huu lugha ilionekana kuwa na viambajengo kama vile: maneno, kirai, kishazi na sentensi na kwamba viambajengo hivyo vina uhusiano mkubwa na viko katika kidarajia toka chini hadi juu. Kwa mfano
        Mkulima bora analima vizuri
Katika sentensi hii kuna uhusiano wa karibu wa viambajengo vifuatavyo; N+V yaani nomino “mkulima” na kivumishi “bora”, hali kadhalika, T+E, yaani kitenzi “analima” na kielezi “vizuri”.
Katika mkabala huu dhana ya uchamko ikaibuka kuonyesha uwezekano wa kuzalisha sentensi bila kufika kikomo. Kwa mfano,
       Waziri fisadi amekamatwa jana na rais akiiba fedha za wananchi.
Hivyo ili kuwa na nadharia inayokubalika katika jamii ni muhimu kuzingatia fasili ya Sengo, (2009:1) ambaye anasema kuwa “nadharia ni wazo kuu, fikra kuu, mwongozo mkuu wa mtu, watu au jamii ya pahala fulani, wakati fulani na kwa sababu fulani”.
Kwa mantiki hiyo nadharia ni dira au mwongozo wa kulikabili jambo kifalsafa, kidini, kimantiki, kijamii na kiutamaduni.
              Kwa ujumla nadharia huchukuliwa kuwa ni dira ya kumwongoza mtafiti au mchambuzi kulikabili na kulielezea vyema jambo fulani kwa mtazamo unaotazamiwa kuwa imara zaidi kuliko ule wa nadharia nyingine. Nadharia hutoa mwongozo katika utatuzi wa jambo fulani ambalo halijaweza kuhakikishwa ukweli wake. Ni mawazo , maelezo au mwongozo uliopangwa ili kusaidia kutatua au kutekeleza jambo fulani kifalsafa, kidini, kimantiki, kijamii na kiutamaduni.


             MAREJEO
http://nenothabiti.blogspot.com/p/fasihi.html by Anonymmous Said, 31 October 2013 at 9:39AM
Sengo, T.S.Y.M (2009) Fasihi za Kinchi. Dar es Salaam: The Trustees of Al Amin Education and Research Academy
TUKI (2004). Kamusi ya Kiswahili Sanifu. Dar es salaam: TUKI
Wamitila, K.W (2003) Kichocheo cha Fasihi Simulizi na Andishi. Nairobi: Kenya Focus   Publications Ltd
Wafula, R.M & Njogu, K (2007) Nadharia za Uhakiki wa Fasihi. Nairobi: Jomo Kenyatta Foundation