SIBANDUKI
Kama kidole na Pete,
Au ulimi na mate,
Milele takuwa wote,
SIBANDUKI.
Mapigo yenda ta ta ta,
Mie kwako ni zezeta
Wala siwezi kujuta,
SIBANDUKI.
Mtasema msemavyo,
Kuchongea mjuavyo,
Nitabaki hivyo hivyo,
SIBANDUKI.
Tumependana wenyewe,
Tunapeana wenyewe,
Tunafurahi wenyewe,
SIBANDUKI.
Waongee Siku kucha,
Penzilo halitochacha,
Daima sitakuacha,
SIBANDUKI.
Waseme maneno yote,
Ya duniani kote,
Hadi wakauke mate,
SIBANDUKI.
Kiangazi na masika,
Siku mwezi na miaka,
Kwa kimbunga na ghalika
SIBANDUKI.
Hata nichomwe mikuki,
Au risasi lukuki,
Kwako mwandani sing'oki,
SIBANDUKI.
Mahakama za kitaifa,
Au za kimataifa,
Waninyonge hadi kufa,
SIBANDUKI.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni